Kama wewe umekuwa ni msomaji wa tovuti ya Tanzania Tech, lazima unajua kuwa tulisha angalia kuhusu nchi zenye kasi kubwa ya Internet duniani pamoja na Afrika kwa ujumla. Kwa muda huo tafiti zilikuwa ni za muda kidogo lakini sasa ni wakati ufahamu kuhusu Afrika na nchi zenye kasi kubwa ya internet ya waya kwa mwaka huu (2018).
Kwenye tafiti hii mpya ambayo imefanywa na mtandao wa Cable, nchi ya Madagascar ambayo inasemekana ni moja kati ya nchi masikini duniani, sasa inaongoza kwa kuwa na internet ya waya yenye kasi zaidi barani Afrika.
Kwa mujibu wa tovuti ya Quartz, kwa sasa Madagascar inaongoza kuwa na kasi kubwa ya internet na hadi kupita nchi kama za Ulaya, Ufaransa na hata Canada. Ikiwa na kasi ya internet ya waya (broadband) ya hadi MB 24.9 kwa sekunde, Madagascar inashikilia nafasi ya 22 dunia huku kwa hapa Afrika ikiwa inashikilia nafasi ya kwanza na kufuatiwa na nchi ya Kenya ambayo mwaka uliopita ilikuwa ikiongoza. Hata hivyo kwa mujibu wa Atlas, kwa sasa hizi ndio nchi za Afrika zinazoongoza kwa kasi ya Internet.
Nchi za Afrika Zenye Kasi ya Internet Mwaka (2018)
- Madagascar – MB 24.9 kwa Sekunde
- Kenya – MB 10.1 kwa Sekunde
- Afrika Kusini – MB 6.4 kwa Sekunde
- Cape Verde – MB 3.2 kwa Sekunde
- Ghana – MB 2.9 kwa Sekunde
- Zimbabwe – MB 2.9 kwa Sekunde
- Rwanda – MB 2.6 kwa Sekunde
- Namibia – MB 2.6 kwa Sekunde
- Burundi – MB 2.6 kwa Sekunde
- Uganda – MB 2.4 kwa Sekunde
Kwa mujibu wa tovuti ya Quartz, Madagascar inaongoza kwa kasi ya internet Afrika kutokana na mkongo wa East African Submarine Cable System (EASSy) ambao pia unapita Tanzania wenye urefu wa km 10,000 ambao unatoka Sudan hadi Afrika ya Kusini.


