Mfumo wa Android Wafikisha Miaka 10 Toka Kuanzishwa Kwake

Hii hapa historia kamili ya mfumo wa Android
historia ya android historia ya android

Mfumo wa Android ni moja ya mfumo ambao unatumika kwenye simu nyingi sana kwasasa, mfumo huu kwa sasa unamilikiwa na kampuni ya Google na hapo siku ya jana mfumo huo umefikisha miaka 10 toka kuanzishwa kwake rasmi.

Sasa kwenye miaka 10 hii ya kuanzishwa kwa Android labda nikupe historia kidogo ya mfumo huu ambao sasa ndio unaonekana kutumiwa zaidi kwenye simu za mkononi maarufu kama smartphone. Kwa kuanza labda tuanzie mwaka 2005 ambapo mwaka huu kampuni ya Google ndio ilinunua kampuni ya Android Inc ambayo ndio ilikuwa mtengenezaji wa mfumo huo.

Kampuni hiyo ya Android Inc ilikuwa ikiongozwa na kumilikiwa na Andy Ruby, Rich Miner, pamoja na Nick Sears ambao ndio waanzilishi na wabunifu wa mfumo huu. Kampuni ya Google ilifanikiwa kununua kampuni ya Android Inc kwa makadirio ya dollar za marekani $50 Milioni ambayo ni sawa na Tsh Bilioni 1.14. Mbali na kiasi hicho, kwa mujibu wa tovuti ya venturebeat inasemekana kampuni ya Google ilitumia zaidi ya dollar za marekani $ 130 milioni kuweza kukamilisha ununuzi kamili wa kampuni ya Android Inc.

Advertisement

Baada ya Google kufanikiwa kununua kampuni hiyo inayochipukia ya Android Inc, Mwaka 2007 kampuni ya Google ilitangaza rasmi kuleta mfumo huo rasmi kwa watumiaji mbalimbali. Kufanikisha hayo simu ya kwanza yenye kutumia mfumo wa Android ilizinduliwa rasmi tarehe 23 mwezi September mwaka 2008 kwa ushirikiano wa kampuni tatu za Google, T-Mobile, pamoja na HTC.

HTC Dream au G1 ndio jina la simu hiyo ya kwanza iliyokuwa ikitumia mfumo huo wa Android kwa mara ya kwanza kabisa, simu hii kama wewe ni muhenga basi lazima kwa namna moja ama nyingine utaikumbuka simu hii. HTC Dream au G1 ilikuja ikiwa na mfumo wa Android 1.6 (Donut), simu hii ilikuwa inauzwa kwa kati ya dollar za marekani $179 hadi $399 na ilikuwa inauzwa rasmi na kampuni ya simu ya T Mobile.

Simu hii ya HTC Dream au G1 ilikuwa na kioo cha inch 3.2 ambacho kilikuwa kimetengenezwa kwa teknolojia ya TFT capacitive touchscreen yenye uwezo wa kuonyesha rangi elfu 65.

Simu hii pia ilikuwa ikitumia processor ya Qualcomm MSM7201A ambayo ilikuwa na nguvu ya MHz 528 pamoja na GPU ya Adreno 130. Kwa upande wa ukubwa wa ndani simu hii ilikuwa na ukubwa wa ndani wa MB 256 huku ikisaidiwa na RAM ya MB 192. Mbali na hayo simu hii ilikuwa na uwezo wa kusoma memory card hadi ya GB 16.

Kwa upande wa kamera simu hii ilikuwa na kamera moja tu ya nyuma iliyokuwa na Megapixel 3.15 ambayo ilikuwa na teknolojia ya autofocus, pamoja na uwezo wa kurekodi video. Battery ya simu hii ilikuwa ni ndogo sana ikiwa na uwezo wa Li-Ion 1150 mAh huku ikiwa na uwezo wa kudumu na chaji kwa masaa 5 pekee.

Baada ya kuzinduliwa kwa simu hii baadae ziliendelea kuja simu nyingine kama Motorola Droid, HTC Droid Eris, Samsung Behold II na HTC Nexus One ambayo ilizinduliwa mwaka 2010.

Kwa ufupi ni kuwa Android kwa sasa ni kubwa sana, hadi kufikia mwaka 2017 Android ilikuwa imeshikilia asilimia 87 ya mifumo ya uendeshaji ya simu janja. Bila shaka asilimia hizi zinaendelea kupanda kila siku huku ukizingatia sasa tuko kwenye mfumo wa Android 9 Pie ambao umezinduliwa hivi karibuni. Kwa sasa mfumo wa Android unaendesha vitu mbalimbali kama vile kompyuta, Radio za magari, TV, pamoja na vifaa mbalimbali vya kielektroniki.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *

Pata Habari za Teknolojia Kupita Barua Pepe

By pressing the Subscribe button, you confirm that you have read and are agreeing to our Privacy Policy and Terms of Use