in

Wizi Mpya wa Fedha Benki kwa Kutumia Wi-Fi Bandia

Tahadhari Imetolewa kuhusu wizi mpya wa fedha benki kwa kutumia Wifi

Wifi ya bure

Habari kutoka gazeti la mwananchi zinasema, Matumizi ya Wi-Fi bandia zinazolingana na Wi-Fi za bure zinazopatikana maeneo tofauti zimeelezwa kuwa chanzo kikubwa cha wizi unaofanywa kwenye akaunti za benki kwa njia ya mtandao. Hilo limebainishwa na kampuni ya kimataifa ya Invostec inayohudumia benki na miradi mingine mikubwa duniani.

Meneja wa idara ya kudhibiti ulaghai wa kampuni hiyo, Kevin Hogan amesema wataalamu wa masuala ya intaneti hutumia mwanya huo kuwaibia wateja ambao hawako makini wanapotumia intaneti hiyo. Kwa kutumia teknolojia ijulikanayo kama man-in-the-middle (MITM) au ‘mtu wa kati’, Hogan amesema watalaamu hao huchukua taarifa za mteja anayetumia Wi-Fi yao kuingia kwenye akaunti yake ya benki kuiba fedha alizonazo.

Install Android App
Price: Free
  • Nyimbo Mpya Screenshot
  • Nyimbo Mpya Screenshot
  • Nyimbo Mpya Screenshot
  • Nyimbo Mpya Screenshot
  • Nyimbo Mpya Screenshot

“Kufanikisha uhalifu wao, hutengeneza Wi-Fi inayofanana na rasmi iliyopo kwenye eneo husika. Kama upo Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa OR Tambo kwa mfano, na Wi-Fi yake halisi ni OR Wi-Fi ambayo nenosiri (password) yake ni ORpass mhalifu hutengeneza yake na kuiita OR Free Wi-Fi na kutumia nenosiri linalofanana na la Wi-Fi halisi yaani ORpass,” amesema Hogan.

Kwa kuwa huwa ngumu kwa mteja kugundua tofauti hiyo ndogo iliyopo kati ya Wi-Fi hizo pacha, mteja huingiza taarifa zake za baruapepe ambazo hubaki kwa mhalifu huyo na kumpa uwezo wa kuingia kwenye akaunti ya mteja na kufanya atakavyo. Akizungumza kwenye mkutano wa waandishi wa habari kuhusu uhalifu wa kiuchumi uliofanyika jijini hapa, amesema changamoto yoyote itakayojitokeza kwa mteja pindi anapojiunga na Wi-Fi ya mahali kama vile uwanja wa ndege au hoteli ya kitalii na ukumbi wa mikutano, humshawishi kutumia Wi-Fi pacha ambayo huwa haichelewi kumuunganisha kwenye intaneti.

Mteja anayefanikiwa kujiunga kwenye Wi-Fi hizo anakuwa ametoa taarifa zake muhimu ikiwamo baruapepe na nywila yake hivyo kumpa nafasi mhalifu huyo kusoma barua alizotumia au kutuma, miamala ya benki aliyoifanya na ujumbe mwingine binafsi. “Akishapata taarifa hizi, mhalifu anaweza kuitumia akaunti yako atakavyo. Anaweza kutumia kadi yako ya mkopo (credit card) pia kwani tayari anakuwa anafahamu jina lako kutokana na baruapepe alizozisoma, nakala za vitambulisho, stakabadhi ya mshahara au hawala za fedha,” amesema.

Anaweza asiishie hapo. Hogan amesema mhalifu huyo anaweza programu maalum (spyware) atakayoituma kwenye simu au kompyuta yako ambayo itakuwa inamtaarifu kila kitu unachokifanya. Wizi wa utambulisho, uhamishaji fedha kwa mtandao, mkopo usioutambua na skendo za uwekezaji ni makosa mengine wanayokutana nayo watumiaji wa huduma za benki nchini na kwingineko duniani.

Wi-Fi ni lango la kuingilia kwenye kompyuta yako. Watu wengi ni wahanga wa Wi-Fi za bure kwa sababu hakuna mtu anayetahadhalisha kuzihusu ilhali kuna wahalifu wengi waliopo kwenye eneo hili,” amesema Hogan. Wakati maeneo yenye Wi-Fi za bure yakiongezeka nchini na duniani kwa ujumla, wataalamu wanatahadhalisha juu ya usalama wa wateja hasa wa benki kutokana na uwezekano wa kutoa taarifa binafsi kwa maharamia wa mtandao.

Makala Hii imenakiliwa Kutoka Gazeti la Mwananchi

Wizi Mpya wa Fedha Benki kwa Kutumia Wi-Fi Bandia
Amani Joseph

Tanzania Tech tumejikita kuhakikisha hupitwi na habari yoyote ya teknolojia, endelea kuwa nasi tufuate kwenye mitandao ya kijamii.

Elon Musk Azindua Mfumo wa Akili Bandia (AI) xAI Grok

Written by Amani Joseph

Tanzania Tech tumejikita kuhakikisha hupitwi na habari yoyote ya teknolojia, endelea kuwa nasi tufuate kwenye mitandao ya kijamii.

Toa Maoni Hapa

Kumbuka ni Muhimu Kuandika Jina Halisi na Barua Pepe, Vigezo na Masharti Kuzingatiwa.